Ndege hii ilikuwa inatoka Amsterdam kuelekea Kualar Lumpur

Maafisa nchini Ukraine wanasema kuwa ndege ya abiria iliyoanguka nchini humo ilidunguliwa katika eneo la mashariki mwa taifa hilo ambako waasi wanaoiunga mkono Urusi wamekuwa wakipigana na vikosi vya serikali.


Wanasema abiria wote 298 waliokuwa katika ndege hiyo ya shirika la Malaysia iliyokuwa ikisafiri kutoka Amsterdam kuelekea Kualar Lumpur wamefariki.
Wengi wa abiria hao walikuwa ni raia wa Uholanzi.

Rais wa Ukraine Petro Poroshenko alitaja tukio hilo kama kitendo cha ugaidi.

Maafisa wa Ukraine walichapisha kile walichotaja kuwa mawasiliano ya simu yaliyonaswa kati ya waasi wakiwaeleza maafisa wa Urusi kwamba ni wao ndio waliohusika katika kuindungua ndege hiyo.
Waziri wa mashauri ya nchi za kigeni wa Ukraine, Pavlo Klimkin, amesema kuwa serikali ina ushahidi wa kutosha kwamba ndege hiyo ilidunguliwa.

'Je waasi walihusika?'
'Tulinasa pia mawasiliano ya simu kati ya magaidi hao wakizungumzia kundunguliwa kwa ndege hiyo.Kwa sasa tunatafsiri sauti zao na kisha tutaziweka kwenye mtandao wa internet ili kuthibitisha hilo."


Mabaki ya ndege ya Malaysia iliyodunguliwa

Hata hivyo sauti hizo zilizonaswa bado hazijathibitishwa na upande uliohuru na waasi hao wamekanusha kuhusika wakisema kuwa ni wanajeshi wa serikali ndio walioidungua ndege hiyo

 
Top