SIMULIZI YA KUSISIMUA Sehemu ya Nane
Ilipoishia
“Pumbavu. Unanifanya mimi mjinga sio?” Mama Suzy alifoka.
Kule chini ya uvungu hali ya Ayubu ilizidi kuwa mbaya. Alianza kujuta uamuzi wake aliouchukua wa kumkubalia Suzy. Mapigo yake ya moyo yalikuwa yakimuenda mbio huku kijasho chembamba kikimtoka. Alibana mdomo wake ili kuzuia pumzi zisitoke kwa sauti.
Endelea……
            “Umeanza lini kuvaa nguo za kiume?” mama Suzy alihoji swali ambalo lilipelekea kushusha pumzi kwa Suzy na Ayubu kule chini ya kitanda.
            “Samahani mama. Sitarudia tena”
            “Usifanye ujinga mwanagu si unajua kuwa nakupenda” Mama Suzy alisema kwa upole.
            “Ndio mama” alijibu Suzy kwa upole. Mama Suzy alitaka kuondoka lakini alipofika mlangoni alirudi tena.
            “Kuna mkebe ulikuwa huku chini ya uvungu” alisema mama Suzy huku akitaka kuinama kuchungulia chini ya mvungu. Suzy alimuwahi na kuinama yeye.
            “Ngoja nikusaidie mama” alisema Suzy na kuinama. Lakini alitafuta kile kimkebe bila ya mafanikio. Alimkonyeza Ayubu na kumwambia atulie kimya. Suzy alipokikosa kile kimkebe alitoka.
            “Mama sijakiona”
            “Basi ngoja nikiangalie mwenyewe” alisema mama Suzy akitaka kuinama.
            “Nimekumbuka mama”
            “Nini?”
            “Nilifanya usafi na kukipeleka stoo” Suzy aliongopa.
            “Haya nenda ukanitafutie” Alisema mama Suzy huku akiondoka. Mama Suzy al;ipotoka Suzy alijibwaga kitandani na kupumua kwa nguvu. Hakuamini kama mama yake ametoka pasipo kugundua kitu kilichokuwa kikiendelea. Ayubu alimgusa Suzy mguuni ili kujua kilichokuwa kikiendelea. Suzy aliinuka na kuelekea mlangoni na kuchungulia nje. Alipoona hapakuwepo na mtu alimpa Ayubu ishara ya kutoka. Ayubu alifanikiwa kuingia chumbani kwake bila kuonekana. Hakuweza kuamini kama amepona kutoka kwenye mdomo wa mamba.
                                                            ****
Maisha ya Ayubu na Suzy yalibadilika na kuwa kama vile mtu na mpenzi wake. Wazazi wao walipokuwepo waliitana kaka na dada. Lakini walipobaki wenyewe waliitana majina kama vile Sweety , babe, Honey, Darling, na mengine kadha wa kadha ya kimapenzi. Kila walipopata nafasi waliutumia muda wao kiufasaha. Mapenzi kati yao yalizidi kunawiri huku watu wakiamini kuwa wawili wale walikuwa ni ndugu walioshibana.
            Baada ya miezi mitatu tangu walipoanza mchezo wao Suzy alianza kubadilika. Alionekana akinawiri, huku matiti yakiongezeka ukubwa. Alikuwa na kila dalili ya kuwa na ujauzito. Alipojigundua kuwa amenasa alimfahamisha haraka Ayubu.
            “Ayubu”
            “Niambie mpenzi”
            “Nina tatizo”
            “Tatizo gani? Ayubu alihoji kwa mashaka. Kitu kilichomshangaza ni kwamba Suzy alikuwa akilia badala ya kuzungumza.
            “Sasa kama unalia mi ntakusaidiaje?”
            “Nina…nina…nina ujauzito Ayubu” alisema na kuanza kulia kwa sauti.
            “Mungu wangu!! Una….una mimba! Nimekwisha” Ayubu alihamaki huku ameweka mikono kichwani. Alionekana kuchanganyikiwa asijue cha kufanya. Taswira ya matatizo aliyokumbana nayo punde alipoingia jijini ilimjia tena. Tatizo lililomkuta safari ile akaliona ni kubwa zaidi, alifahamu kuwa uhai wake ulikuwa matatizoni endapo Mzee Manyama angeligundua lile. Aliinua macho na kumtazama Suzy usoni.
            “Suzy, baba yako ataniua”
            “No! sitakutaja”
            “Kweli Suzy?”
            “Nakupenda sana Ayubu, siwezi kukutaja”
            “Nashukuru sana Suzy. Hata mimi nakupenda” alisema Ayubu na kumkumbatia Suzy.
Pamoja na kwamba Suzy alimuahidi kuto kumtaja kwa baba yake, lakini Ayubu moyo wake ulipoteza amani kabisa. alikuwa akiwaza na kuwazua kitu ambacho kingetokea endapo baba yake Suzy angegundua suala lile. Kuna wakati alipata wazo la kutoroka lakini ahadi aliyopewa na Suzy ya kuto kumtaja ilimpa moyo wa kuvumilia.
            Siku zilivyozidi kwenda Suzy naye ndivyo alivyozidi kubadilika. Hatimaye wazazi wake waligundua hali ile. Mama Suzy alimuita mwanawe kwa urafiki na kumuuliza mtu aliyehusika na ujauzito ule lakini Suzy alionekana kuwa mgumu kumtaja. Baada ya sauti ya upole kushindikana ilibidi ukali utumike. Mama Suzy alifoka huku akimtandika makofi binti yake kumlazimisha amtaje mhusika wa lile tukio. Kelele za mama Suzy zilimgutusha Ayubu ambaye alikuwa chumbani kwake amepumzika. Ilimbidi kutoka na kusimama mlangoni kwa Suzy kusikiliza kilichokuwa kikiendelea. Alipogundua kuwa alikuwa akiadhibiwa kwa kugoma kumtaja mtu aliyempa ujauzito, Ayubu alirudi chumbani kwake na kujiweka tayari kwa matokeo yoyote.
            Wakati mama Suzy alipokuwa akimfokea mtoto wake mzee Manyama alikuwa anarejea kutoka kazini. Alisimama pale mlangoni kusikiliza muelekeo wa mazungumzo yale. Alipogundua kuwa lilikuwa suala la binti yake kupewa ujauzito alifungua mlango na kuingia bila kubisha hodi. Walipomuona wote wawili walishituka, mama Suzy akajibaraguza ili mume wake asigundue.
            “Kuna nini?”
“Hakuna kitu mume wangu”
“Pumbavu, unafuga maradhi? Nimesikia kila kitu” alisema Mzee Manyama huku ameshika kiuno. Alimtazama Suzy kwa hasira na kujikuta akipumua kwa nguvu.
“Sikiliza we mbwa, Tusipotezeane muda. Sema ni nani aliyefanya huo upuuzi?” mzee Manyama alitoa amri. Alikuwa hapendi kubishiwa alipotaka ufanye kitu fulani. Mama Suzy aliinuka na kwenda chumbani kwa Ayubu na kupaza sauti kumuita. Ayubu moyo ulimpasuka akahisi amekwisha kutajwa.  Alipotoka mama Suzy alimtuma mtaa wa pili kuchukuwa pesa zake alizokuwa akizidai kwa mama Halima. Lengo la mama Suzy ni kumfanya Ayubu asijue kilichokuwa kikiendelea.
Ayubu alipokuwa akielekea kwa mama Halima alikuwa ametingwa na mawazo. Alifahamu kuwa kurudi kwa mama Suzy ndio ulikuwa mwisho wa maisha yake. Alimfahamu mzee Manyama kuwa alikuwa tayari kupoteza uhai wa mtu kwaajili ya binti yake.
Mama Halima alimpatia Ayubu kiasi cha shilingi Elfu hamsini. Ayubu alianza safari ya kurudi nyumbani kwao. Alipokaribia alisimama na kutafakari cha kufanya. Alipokumbuka ahadi ya Suzy alipata nguvu ya kwenda lakini alipowaza endapo Suzy angemtaja ingekuwaje, hapo nguvu zilimuishia kabisa.
Alikwenda moja kwa moja hadi nyuma ya nyumba na kujibanza akisikiliza kilichokuwa kikiendelea chumbani kwa Suzy. Alimsikia Suzy akilia huku akikataa kumtaja mtu aliyempa ujauzito. Mzee Manyama alipoona Suzy alikuwa akionesha kiburi, alikwenda chumbani kwake na kurudi na bastola. Alimnyooshea Suzy huku akiwa na hasira.
“Heri kuishi bila mtoto kuliko kuishi na mbwa kama wewe. Ayubu anatosha kuwa mtotowetu. Sasa chagua moja kati ya kufa ama kumtaja mtu aliyekupa huo ujauzito”
“Basi….basi….baba…nam…namtaja”
“Mtaje Suzy, utakufa mwanangu” mama Suzy alisihi.
“Ni…ni….ni..A..A…Ayubu”
“What?” Mzee Manyama alihamaki kusikia kuwa Ayubu ndiye mhusika wa ujauzito ule. Kule nje Ayubu moyo ulimpasuka baada ya kusikia jina lake limetajwa. Mama Suzy na mume wake hawakuamini kama kijana waliye muamini na kumpenda angeweza kuwalipa kwa kuwafanyia vile.
“Shukurani ya punda ni mateke. Lazima afe!” alisema Mzee Manyama na kufungua mlango kutoka kwa hasira kwenda kummaliza kijana aliyeharimu maisha ya binti yake.
Itaendelea....
Soma toleo lililopita hapa>>                                     Soma kuanzia Mwanzo hapa>>

Ndugu Msomaji wetu wa Simulizi hii ya Kusisimua, Tupo tayari kukutumia Kila toleo Jipya la muendelezo wake. Kitu cha Kufanya LIKE Uukurasa wetu wa Facebook. Bofya hapa>>
 
Top