Ni kuhusiana na mikataba mbalimbali aliyoingia.


Mwanza. Chadema kimesema kinaishanga Serikali kumtoa sadaka aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka na kumuacha Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo akiendelea kutumia fedha za umma kwa kuzunguka mikoani.
      Pia, chama hicho kimehoji kuwa Profesa Tibaijuka na mikataba ya nishati ni wapi na wapi na kwamba kumuacha Profesa Muhongo bila kumuwajibisha ni kuendelea kuifanya Serikali izidi kuchukiwa na wananchi bila sababu ya msingi.
      Akihutubia kwenye mkutano wa hadhara juzi uliyofanyika kwenye Viwanja vya Furahisha na kuhudhuriwa na mamia ya wakazi wa mkoa huu, naibu Katibu mkuu wa chama hicho Zanzibar, Salum Mwalimu alisema Serikali kuendelea kumuacha Waziri wa Nishati na Madini ni jambo la ajabu, kwani yeye ndiye mtu aliyepaswa kuwajibishwa awali.
      “Unajua kitu tunachokiona hapa ni jambo la kushangaza. Mhusika mkuu wa mambo yote yanayohusu mikataba ya nishati anaachwa halafu mtu anayeshughulikia masuala ya ardhi anakuwa mtu wa kwanza kuwajibishwa kama siyo kumtoa sadaka ni nini,” alihoji Mwalimu.
      “Leo Profesa Muhongo anaendelea kutumia fedha za umma kwa kuzunguka mikoani na kutoa ahadi ambazo hawezi kuzitekeleza. Chadema hatutakubali kuona CCM inaendelea kuwanyonya wananchi, lazima mabadiliko ya kweli ya fanyike mwaka huu,” alisema.
      Naibu katibu mkuu huyo wa Chadema Zanzibar alisema wamekuwa wakiona na kusikia kwamba kuna viongozi wa juu wa CCM wamekuwa wakija Mwanza kwa madai ya kuweka mikakati ya kukomboa majimbo yanayoongozwa na Chadema, lakini watambue majimbo hayo hayatarudi kwao.
     Mwalimu alisema kila mbinu zinazofanywa na CCM kipindi hiki wanazitambua na kwamba chama chao kipo imara kila idara, kwani picha nzuri tayari wameionyesha kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa.
         “Tunajua kuna vigogo wa CCM wamekuwa wakija Mwanza, kwa madai ya kutaka kuja kukomboa majimbo yaliyochukuliwa na Chadema, lakini tambue wao wakiwaza kufanya hivyo sisi tumeshawaza mbele zaidi na picha wameiona kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa.”
      Aidha, Mwalimu alipinga hatua ya Tume ya Uchaguzi kuruhusu jeshi kusimamia Uchaguzi Mkuu mwaka huu, huku akieleza kuwa kazi ya jeshi ni kulinda mipaka siyo uchaguzi.
      Mwalimu jana aliwatembelea wafuasi wa chama hicho waliopo kwenye Gereza la Magu, ambao waliokamatwa kwa madai ya kufanya vurugu. 
 Crdt: Mwananchi
 
Top