“Hivi inaingilia akilini kweli kwa mfanyakazi TRL unasimamisha treni na kuiba mafuta? Ninadhani haingiii akilini hiki ndicho walichokifanya baadhi ya niliowafukuza wenzenu.” Dk Mwakyembe

Dar es Salaam. Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe amewafukuza kazi wafanyakazi sita wa Shirika la Reli Tanzania (TRL) na kuamuru wakamatwe na polisi kwa tuhuma za kuhujumu shirika hilo.


Mbali na uamuzi huo, pia Dk Mwakyembe ameigiza Bodi ya TRL kuanzia jana kusitisha mkataba na Kampuni ya Translog inayojihusisha na upakuaji na kuhesabu mizigo katika treni, badala yake kazi hiyo ifanywe na wafanyakazi wa shirika hilo.


Akizungumza jana katika mkutano na wafanyakazi, Dk Mwakyembe alisema kuwa wizara yake haiwezi kuvumilia hujuma na wizi unaofanywa na watumishi wachache wasio waaminifu.


“Kila siku nimekuwa napambana Waziri wa Fedha Saada Mkuya ili awaongezee mishahara, lakini nakutana na hivi vituko vya wizi kutoka kwa baadhi ya wafanyakazi wenzenu,” alisema Dk Mwakyembe.


“Nina ushaidi wa video jinsi baadhi yao walivyohusika na jambo hili, nimechoka kupiga siasa na wakishakamatwa nataka uchunguzi wa mali zao uanze mara moja na ikiwezekana zipigwe mnada,” alisema. 


Aliongeza: “Kibaya zaidi, kuna wafanyakazi ambao kazi kubwa ilikuwa kukatisha tiketi kwa abiria kwa Sh61,200, lakini cha ajabu kiasi kinachoingia TRL ni Sh16,000 huu si wizi.”


Kuhusu Translog Dk Mwakyembe, aliigiza Bodi ya TRL kusitisha mkataba huo alilodai unainufaisha kampuni na shirika hilo likishindwa kupiga hatua za maendeleo kama miaka ilivyopita.


“Shirika lenyewe bado linajikongoja, halafu  bodi bado mnang’ang’ania kufanya kazi na kampuni hii. Kuanzia leo, sitaki kuona fedha yoyote inayotoka TRL kuwalipa Translog na atakayefanya hivyo tutamkata kwenye mshahara wake,” alisema Dk mwakyembe.


Katika hatua nyingine, Dk Mwakyembe amemwagiza katibu mkuu wizara hiyo, Shaaban Mwinjaka kuungana na timu ya watu wanne ya wataalamu kutoka idara mbalimbali, ikiwamo Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuchunguza mabehewa mapya matatu yaliyoanguka hivi karibuni na jana mkoani mkoani Morogoro.


Awali, Katibu wa Chama cha Wafanyakazi wa Reli (Trawu) John Kiwele alisema hatua hiyo ya waziri ya kuwafukuza kazi watumishi wasiowaaminifu  ni nzuri na alitaka uchunguzi wa kina ufanyike katika ununuzi wa mabehewa ambayo alidai kuna harufu ya rushwa ndani yake.
 Kutoka Mwananchi
 
Top