Wanafunzi waliokuwa kwenye maandamano ya kudai fedha zao za kujikimu walidai kuwa kuna baadhi ya wanafunzi wenzao waligongwa na gari ya polisi iliyokuwa ikitawanya maandamano hayo ambayo polisi waliyaita ni haramu na kufariki dunia.

Kufuatia uvumi ulioenea katika mitandao mbalimbali ya kijamii na katika mji wa Dodoma na viunga vyake kuwa kuna wanafunzi waliofariki dunia kufuatia maandamano yaliyofanyika juzi katika Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom), Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma, Dk Nassor Mzee amesema kuwa taarifa hizo si za kweli.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana mjini hapa, Dk Mzee amesema kuwa hakuna maiti yoyote ya mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma iliyopokelewa katika hospitali hiyo na kusisitiza kuwa taarifa hizo siyo za kweli.

“Hapa hospitalini hakuna maiti yoyote ya mwanafunzi wa Udom na hata baada ya kupata taarifa hizo nilikwenda mapokezi kwa ajili ya kupata taarifa na kwenye wodi zote hapa hospitalini lakini hakuna mwanafunzi hata mmoja wa kutoka Udom aliyefika hapa kutibiwa,” amesema Dk Mzee.

Aliongeza kuwa, “Hata kwenye chumba cha kuhifadhia maiti hakuna maiti yoyote ya mwanafunzi wa udom… labda kama waliamua kwenda kuzihifadhi maiti hizo kwenye hospitali nyingine nje ya hapa lakini hapa hakuna maiti yoyote kutoka Udom.”

Awali baadhi ya wanafunzi waliokuwa kwenye maandamano ya kudai fedha zao za kujikimu walidai kuwa kuna baadhi ya wanafunzi wenzao waligongwa na gari ya polisi iliyokuwa ikitawanya maandamano hayo ambayo polisi waliyaita ni haramu na kufariki dunia.

Pia katika taarifa yake kwa vyombo vya habari iliyotolewa juzi na jeshi la polisi haikutaja vifo wala majeruhi zaidi ya kutaja idadi ya wanafunzi waliotiwa mbaroni kufuatia maandamano hayo kuwa ni 84. 
Kamanda wa polisi Mkoa wa Dodoma, David Misime alisema kuwa wanafunzi wote waliokamatwa katika maandamano hayo wameshafikishwa mahakamani kujibu mashtaka yanayowakabili ya kuvuruga amani chuoni na kufanya maandamano haramu.
 
Top