BONGO DAS'LAAM Sehemu ya 3
Ilipoishia....
        “Hembu lifunue” sauti ya mtu yule ilizidi kumshitua Ayubu na kumfanya atetemeke. Alifahamu wazi kuwa watu wale waliokuwa na silaha zilizokuwa zimelowa damu, wasingeweza kumuacha akiwa hai.
      Ayubu alifumba macho na kumuomba Mungu atende miujiza. Yule mtu aliyeambiwa afunue tenga aliliangalia kitambo kisha akaligongagonga kwa ule mguu wake.
Endelea....

            “Hakuna sababu ya kulifunua. We weka mzigo tusepe”
            “Basi angalia kama kuna mtu anatuona”
            “Hakuna bwana, hembu wacha woga”
         “Inabidi kesho tuhakikishe mteja anapatikana” alisema yule mwengine na kutoa kifuko kidogo na kukichomeka kwenye lile tenga. Alishituka baada ya kumgusa Ayubu kwenye mgongo.
           “Mnh!”
           “Vipi?”
           “Hapa kuna mtu nini!”
           “Kwani vipi?”
           “Kuna kitu kigumu”
           “Achana nacho, weka mzigo wetu tuondoke. Mtu hawezi kakaa hapo”
Watu wale baada ya kuficha kale kamfuko kao walielekea upande wa pili wa maeneo yale. Ayubu alitulia kwa muda mrefu hadi alipobaini kuwa hapakuwepo na mtu  mahali pale. Alijitoa taratiibu kutoka kwenye lile tenga. Alichukua kile kifurushi kilichokuwa kimefichwa na wale watu. Alipokifungua hakuweza kuamini macho yake. Yalikuwa ni madini ya dhahabu, kitu ambacho kilimsababisha kuwacha masomo na kwenda mgodini.
            Hakutaka kuchelewa, alikitumbukiza kwenye nguo ya ndani na kuondoka haraka kuelekea kule walikotokea wale watu. Akili yake ilikuwa ikiwaza utajiri. Alijiona ni kiasi gani Mungu amempendelea kwa kumpa utajiri akiwa bado kijana mdogo vile. Taswira ya jumba kubwa la kifahari na magari ya kifahari ilimjia akilini mwake.
            Alipata nguvu ya kutembea kwa muda mrefu ili kutafuta mahali pa kulala usiku ule ambapo ni mbali na maeneo yale. Alikwenda kujilaza pembeni ya duka moja kubwa la sonara. Aliamini maeneo yale pasinge kuwepo na mtu yoyote ambaye angemfanyia kitu kibaya kwasababu palikuwa peupe. Hivyo ingekuwa rahisi kuomba msaada hata kutoka kwa walinzi wa maduka.
            Alitandika kirago na kujilaza, aligalagala kwa muda mrefu pasipo kupata usingizi. Mara ilifika gari ya polisi na askari watu walishuka. Ayubu alishituka na kutaka kukimbia kutokana na jinsi askari wale walivyoshuka kwa mbwembwe kutoka kwenye gari. Walimzunguuka Ayubu na kuanza kuongea nae.
              “We kijana, unafanya nini hapa”
              “Nime….nime….nimejipumzisha Afande”
              “Wewe ni mwizi”
              “Ha…ha…ha…hapana”
         “Msirichereweshe Afande. Rireteni turipereke. Riuaji hiro”  alisema askari aliyekuwa kwenye gari kwa msisitizo.
Ama kweli “kama haipo haipo tu” kwenye lile duka la sonara alilokuwa amelala Ayubu, kulikuwa kumevunjwa na kufanyika kitendo cha wizi. Mbaya zaidi watu walioiba wamefanya mauaji ya mlinzi wa duka lile. Askari walianza kufanya upekuzi kwa Ayubu. Laahaula! Alikutwa na kufuko cha dhahabu kwenye sehemu zake za siri.
            “Haaa! We kijana kumbe ni rijambazi?”
            “Jamani sio mimi”
            “Hii umetoa wapi?”
            “Nimeokota, lakini sio hapa”
            “Pumbavu, umewezaje kuua peke yako au unawenzio?”
            “Hapana mimi sijaua jamani” alilalamika Ayubu huku akilia kwa uchungu.
            “Utaozea jera kunguni wee” alisema askari huku wakimnyanyua na kumtumbukiza kwenye gari yao. Ayubu alipigwa virungu kwa kiasi kikubwa. Alijikuta nguvu zikimuishia na kunyong’onyea kutokana na kipigo kile kitakatifu. Ingawa alilia sana na kuomba asamehewe lakini sauti yake haikusikika na hata askari mmoja.
            Gari ilikuwa ikienda kwa mwendo wa kasi sana. Ilikuwa ikielekea kituo kikuu cha Ostabey. Laahaula! Mkosi ndani ya mkosi, kulitokea gari la mchanga ambalo halikuwa na taa na kulivaa lile gari la polisi. Walibingirika mara tatu  na mwisho gali ilisimama matairi yakiwa juu. Ayubu alijua amekwisha poteza maisha. Lakini haikuwa hivyo kwani alitingisha mkono, mguu, na kuchezesha macho bila matatizo. Maumivu aliyokuwa akiyasikia yalikuwa ni yale ya virungu. Kwa ufupi ni kwamba hakuwa ameumia hata kidogo kutokana na ile ajali.
            Siku zote ajali ni kitu kibaya sana, lakini siku ile kwa Ayubu ilikuwa kinyume. Alimshukuru mungu kwa kuwasababishia ajali ile. Askari wote walikuwa wamepoteza maisha pale pale. Alichokifanya ni kujichomoa na kuketi hatua kadhaa kutoka pale kwenye ajali. Alishuhudia maiti za askari zikichomolewa na kupakiwa kwenye gari la kubebea wagonjwa.
            Pale alipokuwa amekaa Ayubu alihisi mtu anamgusa kwenye bega lake la kushoto. Alipogeuka akahisi mapigo ya moyo yakimwenda mbio. Alikuwa ni mmoja wa wale watu waliokuwa wameficha dahahabu zao kule kwenye uchochoro. 
            “Habari yako” Mtu yule alitoa tabasamu na kumsalimia Ayubu.
            “Safi tu, niaje?”
            “Shwari”
            “Nawewe ulikuwepo kwenye ajali?”
            “Amm….ah…hapana sikuwepo”
            “Najua ulikuwepo kwasababu nimekuona ukitoka”
            “Umenifananisha”
            “Sikiliza kijana, ukileta uhuni nawaambia watu wakupeleke polisi. Sema kwanini walikukamata?”
            “Aaah! Wamenionea tu. Lakini sio mimi”
            “Wamekuonea nini”
            “Heti nimeu…..ah! sijui nimevunja duka”
            “Umeiba nini?”
            “Wanasema nimeiba madini”
            “Yako wapi?”
            “Amebaki nayo afande mmoja kwenye gari”
            “Kweli?”
            “Ndio” alijibu Ayubu na kumfanya kijana yule kwenda kwa kasi kwenye lile gari lililopata ajali. Ayubu aliutumia mwanya ule kuondoka maeneo yale. Alihisi kama angeendelea kubaki pale angeweza kutokea mwengine na kumpeleka polisi.
****
Hadi kulipo pambazuka Ayubu alikuwa akitembea. Siku hiyo hakupata kabisa hamu ya kulala tena. Alihisi kuwa ni lazima angeingia mikononi mwa polisi ama vibaka wa jijini kama angelala. Alikuwa ametembea umbali mrefu kutokea pale alipopata ajali usiku. Alikuwa amefika maeneo ya Ubungo.
            Njaa ilikuwa ikimuuma sana kwasababu tangu chakula alichokula mchana siku iliyopita hakutia kitu kingine mdomoni mwake. Aliwaza kitu cha kufanya asubuhi ile ili apate chochote cha kutia mdomoni. Alisogea hadi karibu na mgahawa mmoja uliokuwa karibu yake. Aliingia na kuwakuta watu wakiagiza na kupata kifungua kinywa.  Alimfuata mzee mmoja aliyekuwa amekaa kwenye kona. Mzee yule alionekana kuwa na roho nzuri na sura ya huruma.
            “Shikamoo mzee”
            “Marahaba hujambo?”
            “Samahani mzee wangu”
            “Unasemaje?”
            “Tangu jana sijala naomba unisaidie nipate chochote mzee wangu”
            “Sina hela mimi. Unadhani pesa zinaokotwa?”
            “Nisaidie mzee wangu”
            “We mhudumu hembu njoo utoe hizi takataka zako hapa. Sisi tunakula nyie mnawaachia machizi waje kutusumbua. Vipi bwana!” yule mzee alizungumza kwa ukali. Amakweli umdhaniae ndiye kumbe siye. Kwa muonekano yule mzee alionekana ni mtu mtaratibu sana na mwenye huruma kumbe ilikuwa kinyume. 
                         <<Soma Toleo lililopita                 Soma kuanzia Mwanzo>>                           
  
 
Top