Waziri wa Habari, Utamaduni, Michezo na Wasanii, Nape Nnauye, amewasimamisha kazi, Mkurugenzi wa Idara ya Habari na Matukio wa Shirika la Utangazaji  la Taifa (TBC), Mbwilo Kitujime na Meneja wa Vipindi wa shirika hilo, Edna Rajab.
 
Nape alitoa uamuzi huo alipofanya ziara katika ofisi za shirika hilo zilizoko Mikocheni jijini Dar es Salaam jana.
 
Pia, aliagiza kufumuliwa kwa idara nzima ya habari na matukio ya TBC kutokana na utendaji usioridhisha.
 
Aidha, wakati Nape akifikia uamuzi huo, Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy  Mwalimu, naye amemwagiza Mwenyekiti wa Bodi ya Bohari ya Dawa (MSD), Prof. Idrisa Mtulia, kuwasimamisha kazi mara moja wakurugezi wanne wa bohari hiyo kwa tuhuma za upotevu wa Sh. bilioni 1.5,  akiwamo aliyekuwa Kaimu Mkurungezi, Cosmas Mwaifwani.
 
Wengine waliosimamishwa ni Mkurugenzi wa Fedha na Mipango, Joseph  Tesha, Mkurugenzi wa Ugavi, Misangi Muja na Mkurugenzi wa Manunuzi,  Heri Mchunga.
 
Waziri Ummy alisema uamuzi huo umechukuliwa baada ya uchunguzi  uliofanyika mwaka jana kubaini taratibu za manunuzi zilikiukwa na kuisababishia serikali hasara.
 
Kauli hiyo aliitoa jana katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) alipokuwa akipokea vitanda 120, magodoro 120, vitanda vya kujifungulia 10, vitanda vya watoto njiti 10 na mashuka 420 kutoka kwa Mkurungezi Mkuu wa MSD, Laurean Rugambwa Bwanakunu.
 
Makabidhiano hayo ni utekelezaji wa agizo la Rais John Magufuli kuwa jengo lililokuwa likitumika kama Ofisi ya Kitengo cha Uzazi na Mtoto litumike kuwa wodi ya wazazi Hospitali ya Taifa Muhimbili.
 
“Pamoja na kupokea vifaa  kwa ajili ya wodi ya wazazi, lakini pia viongozi  hao lazima  wasimamishwe haraka ili kupisha uchunguzi ufanyike, hata wafadhili wamesimamisha kutoa fedha za kununulia dawa kutokana na upotevu huo wa fedha,” alisema.
 
Aliongeza kuwa, kabla yeye hajaondoka katika nafasi yake ya uwaziri, wote watakaobainika  kufanya uzembe kwenye manunuzi ya dawa na vifaa tiba baada ya uchunguzi wachukuliwe  hatua.
 
Wakati huo huo, waziri huyo aliwaangiza wakuu wa mikoa na wilaya  kuhakikisha wanapokea taarifa ya idadi ya vitanda na wagonjwa wanaolala chini kila siku kutoka hospitali za wilaya na mkoa ili hatua zichukuliwe haraka.
 
“Namshukuru Rais John Magufuli kwa kutoa msukumo katika wizara ninayosimamia, mimi na Katibu  Mkuu Dk. Mpoki Ulisubisya, hatutalala lazima tutahakikisha taarifa zinapatikana kila siku kutoka hospitali zote nchini,” alisema.
 
“Rais anapotoa agizo hapendi kusikia mchakato, upembuzi yakinifu unafanyika, bali hupenda kuona hatua zinachukuliwa mara moja, hivyo wajawazito wanahamia leo (jana) katika jengo ambalo Rais alihitaji litumike.”
 
Alisema  wafanyakazi wote waliokuwa wakifanya kazi katika jengo lililokuwa MNH, watapelekwa kwenye mamlaka nyingine, ikiwamo  Mamlaka ya Chakula na Dawa Tanzania (TFDA).
 
Awali, akikabidhi vitanda na magodoro kwa Waziri wa Afya, Mkurugenzi  Mkuu wa MSD,  Rugambwa alisema wametekeleza agizo la  Rais Magufuli la kupeleka vitanda katika jengo lililokuwa likitumiwa kama ofisi na wafanyakazi wa Wizara ya Afya.
 
“Tumeanza kuleta vitanda na mashuka  kwa lengo la  kupunguza changamoto ya wajawazito kulala chini katika wodi ya wazazi,” aliongeza kusema.
 Chanzo: Nipashe
 
Top