Waandamanaji wamevamia kituo kimoja cha polisi kinachohusishwa na utekaji na kisha mauaji ya wakili mmoja mteja wake na dereva wa teksi katika kisa kilichotikisa idara ya sheria nchini Kenya.
Waandamanaji walioitikia mwito wa chama cha wanasheria nchini Kenya cha kususia vikao vyote vya mahaka hadi wale waliotekeleza unyama huo wafikishwe kizimbani, walifika kwenye kituo hicho cha Syokimau viungani mwa mji wa Nairobi na kuvamia chumba kinachodaiwa kutumika kuwatesa watatu hao kabla yao kukutana na mauti.
Walikiwasha moto licha ya ulinzi mkali wa polisi waliokuwa wameshika zamu kituoni humo ishara ya hasira inayochemka nchini Kenya dhidi ya mauaji ya watatu hao mikononi mwa walinda usalama.
 
Inadaiwa walizuiliwa kwa muda katika kituo cha polisi wa utawala cha Syokimau.
Miili yao ilipatikana katika mto wa Ol Donyo Sabuk, jimbo la Machakos, mashariki mwa jiji la Nairobi, ikiwa imefungwa mkono na ikionekana kuwa na ishara za majeraha.
Baadhi ya mashirika ya kutetea haki za kibinadamu wanataka mkuu wa Polisi Joseph Boinnet na waziri wa usalama Joseph Nkaissery wajiuzulu.
Kwa mujibu wa shirika lisilo la kiserikali linalofuatilia visa vya ukatili wa polisi dhidi ya raia Kenya la IMLU, mwaka 2015 watu 125 waliuawa kiholela na maafisa wa polisi.

 
Maafisa wanne wanaoshukiwa kutekeleza unyama huo Fredrick Leliman, Stephen Chebulet, Silvia Wanjiku na Leornard Maina wamefikishwa mahakamani na kuwekwa rumande majuma mawili ilikufanikisha uchunguzi.
Uchunguzi wa maiti yao umebaini kuwa walipigwa kikatili na silaha butu kichwani kabla ya kunyongwa.

 
Top