Rais John Magufuli amewateua mabalozi watatu wapya watakaoiwakilisha Tanzania nchi za nje, wakiwamo Dk. Asha Rose Migiro na Mathias Chikawe, ambao alishiriki nao kwenye mchakato wa urais ndani ya CCM.
 
Mbali na Chikawe ambaye jina lake lilikatwa kwenye hatua za awali za mchakato huo, Dk. Migiro aliingia katika hatua ya tatu bora sambamba na Balozi Amina Salum Ali, ambaye alishika nafasi ya pili.
 
Taarifa iliyotolewa jana na Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Gerson Msigwa, ilisema mwingine aliyeteuliwa kuwa Balozi ni Dk. Ramadhan Dau, ambaye ni Mkurugenzi Mkuu wa Mkuu wa Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF).
 
Msigwa ambaye kwenye taarifa yake alikuwa akimnukuu Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue, alisema vituo vya kazi vya mabalozi hao  vitajulikana baada ya taratibu husika za kidiplomasia kukamilika.
 
Hivi karibuni, Rais Magufuli aliagiza kurudishwa nyumbani kwa mabalozi Dk. Batilda Buriani (Japan), Dk. James Msekela (Italia) na Peter Kalaghe (Uingereza). 
 
Sababu za kurejeshwa kwao, kwa mujibu wa Balozi Sefue, ni mabalozi hao na watano kutofanya kazi kikamilifu ya kuiwakilisha nchi kama majukumu yao yanaavyoeleza. Dk. Msekela ilielezwa kuwa mkataba wake ulikuwa umemalizika. 
 
Kutokana na hatua hiyo, vituo vilivyo wazi, ni na Brussels (Ubelgiji) na Kuala Lumpur (Malaysia) baada ya Dk. Diodorus Kamala, kuchaguliwa kuwa mbunge wa Nkenge mkoani Kagera. Kituo cha Kuala Lumpur kiko wazi baada ya Dk. Aziz Mlima kuteuliwa kuwa katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa na Brasilia (Brazil) kutokana na Francis Malambugi kustaafu.   
 
Hii ni mara ya pili kwa Rais Dk. Magufuli kufanya uteuzi wa mabalozi. Mara ya kwanza ulikuwa uteuzi wa Mahadhi Juma Maalim kuwa Balozi wa Tanzania nchini Kuwait, baada ya serikali kufungua ofisi ya ubalozi katika nchi hiyo rafiki. 
 
WASIFU WA MABALOZI WAPYA 
Dk.Asha Rose Migiro
Aliwahi kuwa mhadhiri mwandamizi wa sheria katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam hadi mwaka 2000 alipoingia kwenye siasa na akawa mbunge na baadaye kuwa Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto hadi mwaka 2005.
 
Mwaka 2006 hadi 2007 aliteuliwa kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, akiwa mwanamke wa kwanza kushika wadhifa huo tangu nchi ilipopata uhuru mwaka 1961.
 
Mwaka 2007, aliteuliwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Kimataifa (UN), Ban-Ki-Moon kuwa Naibu Katibu Mkuu wa umoja huo, akiwa mwanamke wa pili kushika nafasi hiyo, ambayo aliishika hadi mwaka 2012 mkataba wake ulipomalizika.
 
Mwaka 2013, Dk. Migoro aliteuliwa kuwa Mkuu wa Chuo Kikuu  Huria cha Tanzania (OUT) na baadaye kuwa Mjumbe wa Bunge Maalumu la Katiba. Baadaye aliteuliwa kuwa Mbunge na Waziri wa katiba na Sheria na Katiba hadi Oktoba, mwaka jana.
 
Dk. Ramadhani Dau
Aliwahi kuwa mwenyekiti wa bodi ya TAN-RE, mjumbe wa bodi ya hoteli ya Serena, benki ya Barclays, Benki Kuu ya Tanzania na Jubilee Insurance. 
 
Pia aliwahi kuwa Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kitivo cha Biashara Idara ya Masoko; Mkurugenzi wa Masoko wa  iliyokuwa Mamlaka ya Bandari Tanzania (THA) sasa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA).
 
Mathias Chikawe
Alianza utumishi wa umma Aprili, 1975 akiwa Mwanasheria wa Serekali Daraja la Tatu katika Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serekali, mwaka 1976 – 1985 alikuwa Mshauri wa Sheria, Wizara ya Kilimo na Mifugo, mwaka  1985 hadi 1988 Ofisa Utumishi Mwandamizi, Idara ya Kanuni za Utumishi Serikalini – Ofisi ya Rais (Utumishi).
 
Mwaka 1988 hadi 1998 aliwahi kuwa Ofisa Utumishi Mkuu na baadaye Mkurugenzi wa Utawala na Utumishi (DAP) kufikia Mkurugenzi wa Huduma za Ikulu, Ofisi ya Rais – IKULU na mwaka 1998 hadi 2005 aliwahi kuwa Katibu Mtendaji wa Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania (LRCT).
 
Mwaka mwaka 2005 hadi 2015 alikuwa Mbunge wa Nachingwea mkoani Lindi na kushika nafasi za Naibu Waziri wa katiba na Sheria (2006  na 2008); Waziri  katika wizara za Katiba na Sheria (2008 – 2010);  Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Utawala Bora (2010- 2012), Kariba na Sheria (2012 -2014) na Mambo ya ndani ya nchi (2014- 2015).
 
WARITHI WA CHAGONJA, KOVA WATEULIWA 
Katika hatua nyingine, Rais Magufuli amempandisha cheo  aliyekuwa Naibu Kamishna wa Polisi Simon Sirro kuwa Kamishna wa Polisi na  kumteua kuwa Kamishna wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es salaam, kujaza nafasi iliyoachwa wazi na Suleiman Kova.
 
Taarifa hiyo pia ilisema Naibu Kamishna wa Polisi Albert Nyamuhanga, amepandishwa kuwa Kamishna wa Polisi na ameteuliwa kuongoza Idara ya Fedha, Utawala na Lojistiki. Anajaza nafasi iliyoachwa wazi na Kamishna Clodwing Mathew Mtweve, aliyeteuliwa kuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Mwanza.
 
Pia Naibu Kamishna wa Polisi Robert Boaz, amepandishwa cheo kuwa Kamishna na ameteuliwa kuongoza Idara ya Intelijensia kujaza nafasi iliyoachwa wazi na Kamishna Valentino Mlowola aliyeteuliwa kuwa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU).
 
Kamishna Msaidizi Mwandamizi Nsato Marijani Mssanzya ambaye amepandishwa cheo kuwa Kamishna wa Polisi, ameteuliwa kuongoza Idara ya Mafunzo na Operesheni, iliyokuwa chini ya Paul Chagonja, aliyeteuliwa kuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Katavi.
 
Wakati huo huo, Rais Dk. Magufuli amemteua Dk. Modestus Kipilimba kuwa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA). 
 
“Kabla ya Uteuzi huu, Dk Kipilimba alikuwa Mkurugenzi wa Menejimenti ya Udhibiti katika Benki Kuu ya Tanzania. Dk. Kipilimba anajaza nafasi iliyoachwa wazi na Dickson Maimu, ambaye uteuzi wake ulitenguliwa,” ilisema taarifa hiyo.
 
Top