POLISI mkoani Rukwa inawashikiliwa watu wawili akiwemo mwanaume anayedaiwa kumbaka na kumyongoa mjamizito Beatrice Kalula (34) mkazi wa kitongoji cha Ichese , Bonde la Ziwa Rukwa wilayani Sumbawanga.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Rukwa ,George Kyando amesema, mwanaume huyo Adrian Maliati (30) na Ester Mwandila (30) walishirikiana kumshambulia na kumnyonga mjamzito huo.

Amesema mtuhumiwa mwingine aliyefahamika kwa jina la Mama Gulo ametoroka baada ya tukio hilo, anatafutwa.

Kwa mujibu wa Kyando, mkasa huo ulitokea Oktoba 4, mwaka huu saa 3:00 asubuhi katika kitongoji cha Ichese, Kata ya Mtowisa, Bonde la Ziwa Rukwa wilayani Sumbawanga.

Imedaiwa kuwa baada ya mwanaume huyo kumbaka mjamzito huyo alishirikiana na wanawake hao wawili kumshambulia kisha kumnyonga na mwili wake kuutelekeza kwenye shamba la Job Malingumu.

“Mwili wa marehemu ulifanyiwa uchunguzi katika kituo cha Afya cha Mtosiwa ulikuwa na jeraha jicho la kulia, michubuko shingoni na damu zilikuwa zikitoka kwa wingi sehemu zake za siri, Chanzo cha mauji hayo bado hakijafahamika ambapo watuhumiwa hao wawili watafikishwa mahakamani" amesema.

 
Top