WATU sita wamefariki baada ya msafara wa Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Suleiman Jaffo na Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Utawala na Serikali za Mitaa kupata ajali wilayani Bagamoyo katika mkoa wa Pwani jana.
Ajali hiyo ambayo ilihusisha magari manne ambayo ni gari dogo aina ya Toyota Blitz lenye namba za usajili T758 DES, lori la mchanga aina ya Scania namba za usajili T738 DCW, Landrover Defender namba za usajili STL 1620 na SM 10414 Nissan Patrol, ilitokea jana saa 5 asubuhi katika eneo la Kerege.
Msafara wa Jaffo pamoja na Kamati hiyo ulikuwa ukitokea katika kata ya Mapinga, kukagua mradi wa maji unaohudumia vijiji vitatu vya Changoela, Mtambani na Mapinga ambako walienda kukagua miradi ya Tamisemi pamoja na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) wilayani humo.
Akithibitisha vifo, Mganga Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Dk Amir Batenga alisema ajali hiyo imesababisha vifo vya watu sita na majeruhi 10 ambao kati yao wanane walipelekwa Hopitali ya Taifa Muhimbili (MNH). Alisema waliopelekwa Muhimbili hali zilikuwa mbaya kutokana na kupata majeraha makubwa.
“Hawa wanane wamepelekwa Muhimbili, lakini mmoja alitibiwa na kuruhusiwa na mwingine alitibiwa na kuchukuliwa na polisi,” alisema Dk Batenga.
Aliwataja waliokufa katika ajali hiyo kuwa ni Mkuu wa Idara ya Mipango na Uchumi wa Wilaya, Hilda Msele (59), Makame Ally (40) dereva wa Tasaf, dereva wa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri wa Wilaya, Khalid Hassan (40), Mwanasheria wa Wilaya, Tunsiime Duncan na Mchumi wa Wilaya Ludovick Pallangyo.
Waliojeruhiwa ni Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya ya Bagamoyo, Ibrahim Matovu, Mhandisi wa Maji wa Wilaya Juliana Msaghaa, Mratibu wa Tasaf Wilaya, Dorothy Njetile na Mweka Hazina wa Wilaya, George Mashauri.
Wengine ni Mshauri wa Tasaf, Amadeus Mbuta, Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii wa Wilaya Julius Mwanganda, Tauliza Halidi na Amari Mohammed ambao ni wananchi na Grace Mbilinyi aliyetibiwa na kuruhusiwa.
Hata hivyo, taarifa zilizopatikana baadaye zilieleza kuwa Mhandisi Msaghaa alifariki akiwa njiani kupelekwa Muhimbili kutokana na kuvuja damu kwa wingi kwani aliumia maeneo ya kichwani. Akizungumzia ajali hiyo, Jaffo alisema Tamisemi imesikitishwa na ajali hiyo kwani imepoteza watu wake ambao ilikuwa ikiwategemea katika utendaji wa majukumu yao.
“Tumepoteza wafanyakazi wetu ambao tulikuwa tukiwategemea kutokana na ajali hii…huku tulikuja kwa ajili ya kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo,” alisema Jaffo.
Hata hivyo, aliwataka madereva kuheshimu na kufuata sheria za barabarani kwani ajali hiyo ilisababishwa na madereva wasiofuata sheria jambo lililosababisha kuvamia msafara huo.
Naye Kaimu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, George Lubeje alisema kutokana na ajali hiyo, kamati yake imelazimika kusitisha ukaguzi wa miradi hiyo ili kutoa nafasi ya kufanya maombolezo ya kuwapoteza watu hao.
Lubeleje ambaye ni Mbunge wa Mpwapwa (CCM), alisema ziara za ukaguzi huo zilikuwa zifanyike katika vijiji vya Mapinga, Chasimba na Buma, lakini imeahirishwa kutokana na ajali hiyo.
Chanzo cha ajali hiyo ni dereva wa gari dogo aina ya Toyota Blitz ambaye alikuwa akitokea Bagamoyo kwenda Dar es Salaam kulipita lori la mchanga katika mlima bila tahadhari na kusimama ghafla baada ya kuona msafara kabla ya lori hilo kumgonga kwa nyuma na gari hiyo kugeukia lilipotoka.
Baada ya kuligonga gari hilo kwa nyuma dereva wa lori alishindwa kulimudu gari hilo na kuligonga gari lingine aina ya Defender mali ya Tasaf na baadaye gari la DED aina ya Nissan Patrol ambalo aligongana nalo uso kwa uso
 
 
Top