WAZIRI wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu amemwagiza Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Bohari Kuu ya Dawa (MSD), kuwasimamisha kazi mara moja wakurugenzi wanne wa taasisi hiyo kutokana na tuhuma za kuwepo matumizi mabaya ya Sh bilioni 1.5.

Wakurugenzi hao ni Mkurugenzi wa Kanda wa MSD, Cosmas Mwaifwani, Mkurugenzi wa Fedha, Joseph Tesha, Mkurugenzi wa Ugavi, Misanga Muja na Mkurugenzi wa Manunuzi, Heri Mchunga.

“Naomba uwaandikie barua za kuwasimamisha wakurugenzi hawa wanne ili wapishe uchunguzi wa matumizi mabaya ya Sh bilioni 1.5 za MSD,” alisema Ummy alipozungumza na waandishi wa habari jana Dar es Salaam.

Ummy alisema taarifa alizonazo ni kwamba kiasi hicho cha fedha, kilitumika kununulia dawa kinyume cha utaratibu na Sheria ya Manunuzi ya Umma, hivyo kuna haja ya kufanyika kwa uchunguzi huo.

Uamuzi wa Waziri huyo wa Afya ni mwendelezo wa hatua kadhaa zinazochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Tano dhidi ya watumishi wa umma ambao wamekuwa wakituhumiwa kujihusisha na vitendo vya ubadhirifu kwa kuchukuliwa hatua katika kile ambacho Rais John Magufuli amekipachika jina la ‘kutumbua majipu.’

Utekelezaji agizo la Magufuli Katika hatua nyingine, Rais Magufuli ya kuwapatia vitanda wanaokwenda kujifungulia katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili jijini Dar es Salaam, jana ilitekelezwa baada ya MSD kupeleka vifaa mbalimbali vyenye thamani ya Sh milioni 89.

Vifaa ambavyo alivikabidhi jana Mkurugenzi Mkuu wa MSD, Laurean Bwanakunu ni vitanda 120, magondoro 120, vitanda 10 vya kujifungulia, mashuka 840 na vitanda kwa ajili ya watoto njiti 10.

“Tumeleta vifaa hivi hapa baada ya kuagizwa na Rais kuwa tulete vifaa hivi kwa ajili ya wodi ya wanawake na Rais ametuhakikishia kuwa fedha hiyo italipwa mara moja,” alisema Bwanakunu wakati akikabidhi vifaa hivyo ambavyo vilipokewa na Waziri Ummy.

Rais alitoa ahadi ya kuwapelekea vitanda wanawake hao baada ya kupita katika wodi hiyo, wakati anatoka kumjulia hali Mufti wa Tanzania, Shehe Abubakary Zubeiry.

Akihutubia Taifa kupitia Wazee wa Dar es Salaam mwishoni mwa wiki, Rais Magufuli aliahidi kuwa ahadi yake ya kuwapelekea vitanda wajawazito hao ataitekeleza haraka.
Akipokea vifaa hivyo, Waziri Ummy alimshukuru Rais kwa kuguswa na afya ya wanawake baada ya kupita katika wodi ya wazazi na kukuta baadhi yao wakilala chini.
Alisema akiwa waziri aliyepewa dhamana ya kuongoza wizara hiyo, amefurahishwa kuona Rais hataki masuala ya urasimu ya mchakato, bali anataka kuona mambo yanatekelezwa kwa vitendo.
“Baada ya kupokea vifaa hivi, nakuagiza Mkurugenzi wa Muhimbili, kwamba vitanda hivi vifungwe leo, na akina mama ambao wamebanana kule wodi ya wazazi wahamishiwe katika jengo lingine ambalo litakuwa na vitanda hivi,” alisema Ummy.
Alisema kwa vitendo alivyoonesha Rais Magufuli, atahakikisha kuwa huduma za afya zinatolewa kwa kiwango ambacho wananchi wanapenda kitolewe.
“Rais ameguswa na matatizo ya wananchi wake, sisi ambao tunamsaidia lazima tuwajibike na amenipa msukumo wa ajabu kushughulikia changamoto zinazozikabili hospitali zetu,” alisema.
Hospitali za mikoa na wilaya kukaguliwa Waziri Ummy alimwagiza Katibu Mkuu wa Wizara yake, Dk Mpoki Ulisubisya kumwagiza Mkurugenzi wa Tiba wa wizara hiyo, ahakikishe anakwenda mikoani kukagua matatizo ya hospitali za mikoa na wilaya na kutoa suluhisho la changamoto hizo.
“Badala ya kwenda nje ya nchi, katibu mkuu mwagize mkurugenzi aende wilayani na mikoani huko akajionee hali halisi za hospitali zetu ili tuweze kushughulikia changamoto hizo,” alisema Ummy.
Pia alimwagiza katibu mkuu kwa kushirikiana na mkurugenzi huyo wa Tiba kutoa taarifa kila siku za hali za hospitali za mikoa na wilaya kama kuna wagonjwa ambao wanalala chini ili watatuliwe matatizo.
Aliwataka wakuu wa mikoa na wilaya kutoa taarifa wizarani kila siku kama katika maeneo yao kuna mgonjwa anayelala chini katika hospitali za wilaya na mikoa. “Sitegemei tena mgonjwa alale chini,” alisema
Chanzo: HabariLeo
 
 
Top