WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye amewasimamisha kazi watumishi wawili wa Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC) kutokana na utendaji usioridhisha.

Akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi za TBC Dar es Salaam jana, Nape aliwataja watumishi waliosimamishwa kazi kuwa ni Mkurugenzi wa Idara ya Habari na Matukio, Mbwilo Kitujime na Meneja wa Vipindi, Edna Rajab ambao wamesimamishwa kazi na uamuzi huo utafikishwa kwa Bodi ya TBC kwa hatua zaidi.

“Tunachukua uamuzi wa kuwasimamisha kazi watendaji hawa ili kujenga upya Idara hii muhimu katika ustawi wa TBC na habari kwa ujumla,” alisema Nape.

Aidha, Waziri huyo amemuagiza Mkurugenzi Mkuu wa TBC kuwachukulia hatua watumishi wengine walio chini ya Idara hiyo kwa kuwa wako chini ya mamlaka yake na kutoa mrejesho wa hatua alizochukua dhidi ya wale wote wilioonesha utendaji mbovu.

Alisema Serikali imefikia uamuzi huo kutokana na kuwepo kwa malalamiko ya muda mrefu juu ya utendaji mbovu na wa kutoridhisha viongozi na baadhi ya watumishi wa Idara hiyo hivyo hatua hizo zimechukuliwa ikiwa ni kujenga upya na kuboresha Idara hiyo muhimu katika uendeshaji wa shirika lolote lile la Habari na kuongeza ufanisi.

Idara ya Habari na Matukio ya TBC inaundwa na Mkurugenzi wa Idara, Meneja wa Vipindi, wahariri na waandishi wa habari.

 
Top