Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako.

Katibu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), Ezekiah Olouch, amesema matokeo ya kidato cha nne yaliyotangazwa hivi karibuni ni batili kwa kuwa Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako, hakuzingatia sheria kufuta mfumo wa wastani wa alama (GPA) kwenda madaraja (division).
 
Kadhalika, amesema waziri alitakiwa kufanya mabadiliko ya kanuni na kuzitangaza katika Gazeti la Serikali (GN) na bila kufanya hivyo upo uwezekano wa wanafunzi kuishtaki.
 
Akitoa maoni yake binafsi kwa Nipashe jana kwa njia ya simu, alisema Sheria ya Baraza la Mitihani kifungu cha 18 kinampa nguvu waziri kutunga kanuni za kupanga matokeo (grading system), lakini waziri huyo kabla ya kutoa tangazo katika GN aliutangazia umma kubadili mfumo wa upangaji matokeo hayo.
 
Alisema Novemba 25, mwaka jana, aliyekuwa Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa, alitoa kwenye gazeti la serikali tangazo la kubadili kanuni za upangaji matokeo kutoka kwenye madaraja kwenda GPA, na kwamba Waziri Ndalichako ameendelea kutumia kanuni hizo na kubadili mfumo.
 
“Kwa hali ilivyo ni wazi kuwa kanuni za kukokotoa matokeo inayoendelea kutumika ni zilizowekwa na waziri wa serikali ya awamu ya nne, hatujaona GN ya Serikali kuhusiana na mabadiliko haya ya sasa, hili limeleta mgogoro mkubwa katika elimu na serikali isipokuwa makini itasababisha wanafunzi kwenda mahakamani,” alisema.
 
Alisema alichotakiwa kukifanya Prof. Ndalichako, ni kutengua kanuni za awali na kuziweka katika GN ili liwe suala rasmi, lakini hakufanya hivyo.
 
“Kutokana na waziri kutotengua kanuni na kutangazwa katika Gazeti la Serikali, naye hajatunga kanuni kwenye mchakato wa sheria, hivyo matokeo ya kidato cha nne ni batili," alisema.
 
Kadhalika, alisema kama hatua ya kuwataka waliopewa matokeo ya GPA warudishe vyeti ni ili kutaka wabadilishiwe kwenda kwenye madaraja, ni kinyume cha sheria, huku akifafanua kuwa hajawahi kuona sheria inafanya kazi kwa kurudi nyuma.
 
Oluoch alisema ili matokeo ya sasa yawe halali ni lazima waziri aheshimu na kufuata sheria na kanuni hata kama kuna sheria namba 20 ya Necta inamruhusu kufanya maamuzi yoyote kuhusiana na baraza hilo, ili kuepuka mkanganyiko na siasa kupenyezwa katika elimu.
 
“Kifungu cha 20 cha sheria ya Baraza la Mitihani ya mwaka 1973 na marekebisho yake, kinasema waziri anaweza kutoa maelekezo ila siyo yanayokizana na kanuni ambazo zipo, alichokifanya waziri ni kukizana na kanuni zilizopo kwa maelekezo yake kwa Necta,” alisema na kuongeza: 
 
“Utungaji wa sheria huwezi ukarudi nyuma, huwezi kusema waliopewa GPA wapewe kwa madaraja, itakubalika kwa sheria ikiwa matokeo kuanzisha madaraja yatafaidisha waliokwisha fahidika na GPA na kuwa na sifa za kwenda vyuo vikuu, vinginevyo mwanafunzi akienda kulalamika mahakamani atasikilizwa kwa kuwa kuna ukiukwaji wa sheria,” alisema.
 
Aidha, alimshauri waziri kuomba ushauri wa kisheria juu ya mkanganyiko huo ili asiitumbukize nchi kwenye mgogoro wa matokeo.
Pia, alisema utaratibu wa kurudisha vyeti utaathiri vyuo vingi ambavyo vilishawapokea wanafunzi wa kidato cha sita waliofanya vizuri chini ya mfumo wa GPA ambao uliwapendelea waliofanya vibaya.
 
Msemaji wa Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Olver Kato, alipoulizwa kama waziri alitoa kwenye Gazeti la Serikali tangazo la mabadiliko ya kanuni, alisema waziri anaishia kutamka na Necta ndiyo wanajua walitumia utaratibu gani kutangaza matokeo, hivyo waulizwe juu ya suala hilo.
 
Katibu Mkuu wa Necta, Dk. Charles Msonde, simu yake haikupokelewa na alivyotumiwa ujumbe mfupi wa maandishi haukujibiwa.
 Chanzo: Nipashe
 
 
Top